ZANZIBAR

RAIS DK. MWINYI AAGANA NA BALOZI MDOGO WA CHINA

FEBRUARI 02, 2024
Border
news image

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi amekutana na Balozi mdogo wa China Mhe. Zhang Zhisheng anayefanyia kazi zake Zanzibar, kumuaga baada ya kumaliza muda wake wa utumishi nchini tarehe 29 Januari 2024, Ikulu Zanzibar.

Aidha Rais Dk.Mwinyi amemshukuru Balozi Mhe.Zhang Zhisheng kwa kudumisha na kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia kati ya Zanzibar na China katika miaka mitatu ya utumishi wake nchini, pia kwa kuratibu vema ziara yake mwaka jana China.

Vilevile Rais Dk.Mwinyi ameeleza kuwa China imeendelea kusaidia Zanzibar na kushirikiana katika miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo sekta ya afya kwa kuleta madaktari kutoka China, ufadhili wa masomo, kujengea uwezo, biashara, utalii, pamoja na kuwepo kwa kampuni za kichina katika kazi za miradi mbalimbali ya miundombinu ya barabara, bandari, na uwanja wa ndege.

Halikadhalika Rais Dk.Mwinyi amewakaribisha wawekezaji kutoka China kwenye sekta ya utalii kujenga hoteli kwa kuongeza watalii zaidi wa Kichina kuitembelea Zanzibar.

Rais Dk.Mwinyi amesema Zanzibar itaendelea kushirikiana na kudumisha uhusiano na China ambayo yametimiza miaka 60.

Naye Balozi Mhe.Zhang Zhisheng amesema China itaendelea kushirikiana na Zanzibar kusaidia miradi mbalimbali ya maendeleo na kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia.

MTV Tanzania